|
Halmashauri ya Jiji la Mbeya kushtakiwa mahakamani
2008-03-24 16:57:54
Na Radio One Habari
Halmashauri ya Jiji la Mbeya itafikishwa mahakamani ikidaiwa fidia ya zaidi ya shilingi milioni 169 kutokana na kuvunja uzio wa kiwanja cha mwananchi mmoja.
Mwananchi huyo ni Bwana Anyimike Mwakanjuki ambaye alikuwa ameanza ujenzi, lakini akavunjiwa kutokana na agizo lililotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Kampuni ya Mwakolo Advocate katika kutekeleza azma ya kuipeleka Mahakamani Halmashauri hiyo imetoa notisi ya siku 30 kutekeleza madai ya mteja wao kwa kumlipa kiasi hicho Bwana Mwakanjuki.
Mhandisi wa Ujenzi Halmashauri ya Jiji la Mbeya Bwana Lingo akizungumza na PST amesema mwananchi aliyevunjiwa alipewa kibali na Mhandisi huyo na kwamba alikuwa hana sababu ya kumkatalia mwananchi huyo kibali cha ujenzi wakati alikuwa amekwisha kamilishiwa taratibu zote na Idara ya Ardhi na Mipango Miji.
Bwana Mwakanjuki amesema uamuzi wake wa kuifikisha Halmashauri mahakamani unatokana na kupeleka malalamiko katika Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo nayo ilimshauri kupeleka suala hilo kwenye vyombo vya sheria ili haki itendeke.
|