|
Tabora waagizwa kufanya mikutano ya hadhara kulaani mauaji ya Albino
2008-05-04 23:18:41
Na Radio One Habari
Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega Mkoani Tabora wameagizwa kufanya mikutano ya hadhara ya kutafuta mbinu za kupambana na kulaani mauaji ya Albino kwenye kata zao.
Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, Bwana Patrick Mbozu alipofunga kikao cha Baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo.
Amesema baadhi ya Albino siku hizi hawatoki nje kwa kuhofia kuuawa na wananchi wenye imani potofu ya ushirikina ambayo wanapandikiziwa na baadhi ya waganga wa jadi.
Ameawaagiza madiwani katika vikao vyao vya maendeleo ya kata kuweka mikakati ya kukomesha mauaji ya albino na kuwaelimisha wananchi kwa kutumia mikutano ya hadhara.
Amesema kwa kuhofia usalama wao Albino wanakuwa wananyimwa haki ya kuishi kwa amani na kinyume cha katiba inayosema kila mtu ana haki ya kuishi na kulindwa usalama wake na mali zake.
|