|
Vijana Kyela waishi kwa hofu ya kulazimishwa kuoa wajane
2008-05-07 19:36:01
Na Radio One Habari
Baadhi ya wananchi wilayani Kyela wamesema vijana wanaishi kwa hofu ya kupoteza maisha na wengine wamezikimbia familia zao kupinga kulazimishwa kurithi wajane.
Wananchi hao wamesema hayo katika mazungumzo na Radio One Stereo wakati wa mkutano uliozungumzia uzazi salama ulioandaliwa na Shirika la Huduma kwa Makazi na watu.
Wamesema pamoja na wanaharakati kupiga vita mila hizo, baadhi ya watu wanaziendeleza na kwamba vijana wanaojaribu kukataa vitendo hivyo, huugua ama kupoteza maisha.
Nao Meneja wa Mpango wa Uzazi Salama-PSI kanda ya Kusini Bwana Angelus Mhelela na Mkuu wa wilaya hiyo Bwana Mashimba Husein Mashimba wamesema elimu imeanza kutolewa kupiga vita mila hiyo ambayo inahatarisha maisha kwa walengwa na kuchangia uzazi usiozingatia mpango.
Wamesema baadhi ya wazazi kwa makusudi wanawakatisha masomo watoto wao, ili kuepuka mzigo wa kusomesha kutokana na kuzidiwa na idadi kubwa ya watoto.
|