|
Hospitali maalum ya Tumbi yapata msaada wa vifaa vya mazoezi ya viungo
2008-05-16 15:44:07
Na Radio One Habari
Hospitali maalum ya Tumbi katika wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imepokea msaada wa vifaa vya mazoezi ya viungo vyenye thamani ya shilingi milioni tatu kwa ajili ya majeruhi wa ajali wanaotibiwa hosptalini hapo.
Shirika lisilo la kiserikali la TRACED linalojihusisha na kusaidia watoto wenye ulemavu limetoa msaada huo na kumkabidhi mkuu wa mkoa wa Pwani Dr. Christine Ishengoma ambaye naye amekamkabidhi Kaimu mganga mkuu wa hosptali maalum ya Tumbi Dr. Andrew Lwali.
Akikabidhi vifaa hivyo katibu mtendaji wa TRACED Bwana Ramadhani Mbonia amesema msaada huo umetolewa kutokana na uhaba mkubwa wa vifaa vya kufanyia mazoezi katika hosptali hiyo inayopokea majeruhi wengi.
Akipokea vifaa hivyo, Kaimu Mganga mkuu wa Hospitali ya Tumbi dr. Andrew Lwali amesema hospitali hiyo imekuwa ikichongesha kwa mafundi seremala vifaa vya mazoezi lakini wagonjwa wanashindwa kutumia kutokana na uzito wa mbao.
|