|
Majeruhi wawili ishara ya dozi Yanga -Chambua
2006-07-09 09:16:57
By Badru Kimwaga
Yanga kuanza mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Bara ikiwa na idadi ndogo ya majeruhi ni ishara ya mafanikio kwa klabu hiyo ya Jangwani, amesema kocha msaidizi Sekilojo Chambua.
Timu hiyo inayoongoza ligi, ina majeruhi wawili tu Gullah Joshua na Thomas Mourice na Chambua amesema huo ni mwanzo mzuri kwani hali za wachezaji hao pia zinaendelea vyema.
Hata hivyo, kocha huyo amekiri kuwa wanatarajia upinzani mkali kutokana na kukamiwa na kila timu.
Chambua alisema juzi Ijumaa kuwa hana wasiwasi na kufanya vema kwa timu yake katika mzunguko wa pili kutokana na jinsi ilivyojiandaa.
Tumedhamiria kutetea ubingwa wetu kwa mara ya pili na ndio maana tunajiamini kwamba tunaweza, ingawa tunafahamu ligi ni ngumu na kila timu inatukamia, alisema.
Aliongeza kuwa kinachowapa msukumo wa kuamini watafanya vema ni kule kuwa na kikosi kizuri chenye wachezaji wenye kujituma na wanaozingatia mafunzo ya walimu wao.
|