|
Netiboli Zenji yasaka m.5/-
2006-07-09 09:17:53
By Mwandishi Wetu
Chama cha netiboli cha Zanzibar, CHANEZA, kinasaka sh. milioni 5, kwa ajili ya kuendesha kozi ya awali ya waamuzi na makocha wa mchezo huo kwa wilaya zake.
Katibu Mtendaji wa CHANEZA, Sharrifa Khamis Sherry alisema katikati ya wiki kwa njia ya simu kuwa kozi hiyo itaendeshwa na wakufunzi wenye kutambuliwa na shirikisho la mchezo huo la kimataifa, Restuta Lazaro na Rahima Bakari.
Fedha tunazosaka ni kwa ajili ya kusaidia kugharamia kozi yetu, kwa kulipia wakufunzi na shughuli nyingine zote za kozi hiyo, alisema Sherry.
Katika hatua nyingine, Sherry alisema ligi kuu ya Zanzibar inayoshirikisha timu nane za wanawake na nne za wanaume, iliyoanza hivi karibuni, itafikia tamati Julai 29, ambapo mzunguko wa kwanza utamalizika Julai 13 kwenye viwanja vya Gymkhana.
Alizitaja timu za wanawake kuwa ni mabingwa watetezi Jeshi la Kujenga Uchumi, JKU, Mafunzo, Afya, Zimamoto, Bandari, Msambweni, Chipukizi na MTS; wakati za wanaume ni mabingwa watetezi Polisi, Nyuki, JKU na Msambweni.
Alisema timu nne za juu kwa wanawake zitashiriki kwenye ligi ya Muungano, ambayo imepangwa kufanyika Tanzania Bara, kwa kushirikisha pia timu za idadi kama hiyo kutoka Bara.
|