|
Wawili waongezwa kikapu cha taifa Arusha
2006-07-09 09:18:29
By Bahati Mollel
Wachezaji Said Akilimali na Malege Emmanuel kutoka timu ya Polisi wameongezwa kwenye timu ya mkoa wa Arusha itakayoshiriki kwenye mashindano ya Taifa ya mpira wa kikapu, ambayo yamepangwa kuanza Julai 17-23 kwenye uwanja wa Ndani wa Taifa.
Mwenyekiti wa Chama cha mchezo huo cha mkoa wa Arusha, ARBA, Ali Juwa alisema hivi karibuni kuwa wachezaji hao hawakuwepo katika kikosi kilichoshiriki michuano ya Miji Mikubwa ya Afrika Mashariki, iliyofanyika katika mji wa Kampala, Uganda hivi karibuni.
Juwa alisema wachezaji hao wameungana na wenzao kwenye viwanja vya Sheikh Amri Abeid kufanya mazoezi chini ya makocha, Kennedy Magoiga na Boniface Millinga.
Alisema Arusha itawakilishwa na wachezaji 12 na viongozi watatu, ambapo wataondoka huko Julai 15 kwa njia ya basi, lakini ameomba wapenzi wa mchezo huo kuwasaidia fedha za nauli kwa timu hiyo, na chama kitatafuta posho.
Hatuna fedha kabisa, tunaomba watu mbalimbali watusaidie kwani tumekuwa katika matatizo ya kifedha kwa muda mrefu, tunataka timu iweze kufika Dar es Salaam kwa ajili ya mashindano hayo, alisema Juwa.
Mbali na Arusha, mikoa mingine ambayo ipo katika maandalizi kamambe ya michuano hiyo, ni mabingwa watetezi Dar es Salaam, Mwanza, Tanga, Mbeya, Morogoro, Kagera, Shinyanga na Tabora.
Tanga inayofundishwa na Frank Masumba na Ahmed Babla, na wasaidizi Mohamed Mwariso na Mohamed Twanga, inafanya mazoezi kwenye uwanja wa Mkwakwani.
|