|
Mambo ma4 yanayotishia ustawi wa Bongo Flava 2007
2006-12-24 09:21:50
By Majuto Omary
Kwamba Bongo Flava imeshika chaneli zote kwa sasa, hilo halina ubishi. Lakini je, mambo yatabaki hivi mwaka ujao na mwaka utakaofuatia?
Hapo ndipo utata ulipo na sijui washikaji zangu, wasanii wa muziki huu wa kizazi kipya, wamejipanga vipi kuikabili hali halisi.
Hadi sasa, Bongo Flava imeonekana kuwa mkombozi wa wasanii. Ndio maana utaona hata waigizaji na wachekeshaji wakiacha fani zao kando na kujitosa kwenye Bongo Flava.
Wanamuziki wa dansi, taarabu, hadi mchiriku,… kila mtu anakimbilia kutoa singo. Na ikishazoeleka kwenye masikio ya watu tu, anatangaza albam kamili iko sokoni.
Mambo ya wasanii wengi yameonekana kuwa safi licha ya vilio vya kulizwa na wadosi na mapromota hapa na pale.
Matamasha yanayoandaliwa mara kwa mara, na shoo za kutumbuiza kwenye shughuli za watu na makampuni si haba zimewatoa vijana wetu, wanapata pesa ya kuweka wese kwenye mabaluni wanayonunua wanapowauzia wadosi haki za albam zao.
Na hata wale ambao nguvu yao haijawa kubwa kiasi cha mauzo ya albam kuwawezesha kununua magari, basi walau mabadiliko machache utayaona kwenye hali zao kimaisha.
Kuna wakati hapa baadhi ya wasanii walikuwa wanakunja si chini ya shilingi milioni moja hadi mbili (kwa mtu mmoja!) wanapoalikwa kutumbuiza kwenye shoo.
Sio wote walifikia matawi ya juu namna hiyo, lakini wengi angalau laki tatu-nne zilikuwa haziwapigi chenga kwa kila shoo.
Lakini kuna dalili kwamba mambo si mazuri kihivyo hivi sasa. Kivipi?
Kwamba jamaa bado wanakula bingo, lakini viwango vya madau vimepungua sana kulinganisha na hali ilivyokuwa mwaka jana, kwa mfano.
Ukikuna kichwa, unaweza ukaorodhesha sababu nyingi tu zilizopelekea neema ya wasanii kupungua:
1. Wingi wa wasanii (na mashabiki wa sanaa wanaojidhania kuwa wasanii) wanaoibuka kila leo.
Yaani kuna watu vipaji sifuri kabisa, lakini wamevamia \gemu\ alimradi wana hela za kwendea studio.
2. Mashabiki kuanza kukinai sanaa inayoonekana haina ubunifu mpya zaidi ya kutumbuiza jukwaani kwa kutumia CD (playback). Wasanii wachache sana wana mastaili na vitu vya kuvutia jukwaani, zaidi ya kuchana mistari tu.
3. Udhaifu mkubwa kwenye ujumbe wa nyimbo. Hapa hata Barizi haihitaji kutia neno. Kila mtu anajua wazi wepesi wa meseji, ama upotoshaji uliojaa kwenye nyimbo zetu.
4. Tabia chafu za baadhi ya wasanii. Hawa wanafanya \samaki wote waonekane wameoza…
Hizi ni baadhi tu ya sababu unazoweza kutaja kuwa zinachangia tishio hili dhidi ya ustawi wa Bongo Flava. Na ndio zimefanya neema ipungue.
Lakini Barizi haitaki kuwatisha washikaji zangu hawa. Mara nyingine gemu huwa ni upepo tu.
Katika muziki ni kawaida kabisa. Yaani inatokea tu mashabiki kama wana uchizi fulani, mara wanaifagilia fani fulani, mara wanaipa mgongo hata kama iko juu bado.
Ila kunapokuwa na tishio kama hili, ndipo \Barizi\ inawauliza washikaji zangu hawa wamejiandaa vipi tunapofunga mwaka 2006 na kukaribisha 2007?
Nadhani wasanii wetu wamejifunza toka kwa masupastaa wa majuu, ambao baadhi wamekuja nchini, kuwa kuna umuhimu wa msanii kutumia kipaji chake kujipatia maendeleo ya ziada nje ya muziki.
Wasanii huko nje wana mastudio yao, makampuni ya usambazaji, na miradi kibao kama ya mavazi na viatu, wakitumia umaarufu wa majina yao kukuza biashara zao nje ya jukwaa la muziki. Juhudi gani wasanii wetu wanafanya kufuata mifano hiyo?
Tukiwa tunafunga mwaka mmoja na kukaribisha mwingine, haya ni mambo \ya akili\ sana kwa wasanii wetu kujiuliza.
Kuna umuhimu wa kuzingatia kuwa gemu siku zote halitabiriki. Leo uko juu, lakini kesho mambo yanaweza yakakubadilikia kabisa. Utafanyaje kama hujajipanga toka mapema?
Twajua si kwamba gemu hili litaanguka leo ama kesho, lakini dhahiri, kila msanii anapaswa kujipanga kivyake, kuwa tayari kukabili hali halisi pale gemu litakapomkataa.
Wakati ndio huu. Jiulize unaingiaje 2007.
|