Alitoa agizo hilo jana alipotembelea na kukagua ujenzi wa soko hilo na Kituo cha Mabasi cha Kisasa cha Nyegezi kilichoko Wilaya ya Nyamagana jijini hapo.
"Nimepata taarifa kwamba msimamizi mmoja anasimamia miradi yote miwili jambo ambalo halikubaliki na linasababisha miradi hii kuchelewa na kuna hatari itatekelezwa chini ya kiwango kutokana na kukosa usimamizi makini," alionya.
Mwanaidi alisema ni lazima msimamizi huyo awapo eneo la ujenzi saa 24 kuangalia ufanisi wa kazi, ili kupata majengo na miundombinu imara itakayosadifu juhudi za Rais John Magufuli, za kujenga miundombinu bora itakayochochea maendeleo ya wananchi.
“Kama msimamizi hakai eneo la ujenzi, basi aondolewe, awaachie wengine ambao wanaweza kufanya kazi hiyo, iwapo msimamizi hayupo, ni vema serikali ikajulishwa ili ichukue hatua stahiki bila kuchelewesha miradi," alisema.
Naibu waziri huyo alitoa siku mbili kwa uongozi wa Wilaya ya Nyamagana kuhakikisha kikwazo cha uhaba wa saruji katika miradi hiyo miwili ya kimkakati inayopewa fedha na Hazina, kinatatuliwa haraka ili kuziwezesha halmashauri kujitegemea kimapato.
Awali, mkandarasi kutoka Kampuni ya Mohamed Builders anayejenga miradi hiyo, Taher Jafferji, alilalamikia kero ya ugumu wa upatikanaji wa saruji licha ya kulipa fedha nyingi kwenye viwanda vya saruji, jambo ambalo linapunguza kasi ya ujenzi.
Alisema amepewa mkataba wa ujenzi wa miezi 18 na anatarajiwa kukamilisha ujenzi wa soko hilo Aprili mwakani, hivyo ni vema serikali ikalitafutia ufumbuzi suala la uhaba wa saruji....kwa habari zaidi fuatilia https://epaper.ippmedia.com