Akizungumza na Nipashe Digital, Mhadhiri Msaidizi wa chuo hicho, Richard Moses amesema hiyo ni moja ya sehemu ya ufundishaji wa Chuo inayohusisha kuwanoa wanafunzi kwa njia ya vitendo.
Amesema wanafunzi hao 50 wanaosomea Shahada ya Usanifu Majengo watakaa visiwani humo kwa siku 14 wakijifunza masuala mbalimbali ya usanifu.
Amesema ingawa wanafunzi hao wanasomea usanifu kwa majengo mapya lakini wanalazimika kupata ujuzi kuhusu majengo ya kale kwa kuyapima na kuyarekodi ukubwa wa majengo na yalitumikaje.
“Wanachunguza majengo haya yalipitia matumizi gani mpaka leo hii na pia watapendekeza mabadiliko ambayo yanapaswa kufanywa kwa majengo hayo ili yaendelee kutumika kwa miaka mingi hivyo watajifunza kwa vitendo kuhusu majengo ya kale,” amesema Mhadhiri huyo.

Amesema lengo kubwa hasa la kuwapeleka visiwani Zanzibar ni kuwajengea uwezo wa kuweza kukabiliana na soko la ajira kwa kujua masuala mbalimbali kwa vitendo hivyo kuwaongezea ujuzi.
“Wakiwa hapa Zanzibar wanafunzi hawa wameweza kufanya tathimini katika mji mkongwe maarufu kama ( Stone Town) kwa kupata historia yake, matumizi ya jengo wakati wa zamani na sasa, aina ya ujenzi uliotumika, thamani, na vipimo mbalimbali kwa kuendana na wakati husika,” amesema.
Amesema pamoja na hilo taarifa hizo zinaweza kusaidia kutumika na wataalam mbalimbali hasa kwenye kushauri au kupendekeza juu ya matumizi, thamani na matumizi endelevu ya majengo hayo kongwe kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
