Bajeti ya Wizara ya Elimu kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ina kauli mbiu inayosema 'Elimu ujuzi ndio mwelekeo' ikiwa na maana msisitizo na mkazo katika mitaala yetu utajikita zaidi katika kuhakikisha wahitimu wanakuwa na ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiri wengine.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia,Prof. Adolf Mkenda, amesema Serikali imetoa ufadhili kwa wanafunzi 1,220 kati ya 1,200 waliolengwa (wanafunzi wapya 915 na wanaoendelea 305) wenye jumla ya Shilingi Bilioni 6,367,169,632 kupitia Samia Scholarship.
"Serikali imekamilisha Mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 na kuandaa Sera ya Elimu na Mafunzo 2014, Toleo la 2023. Vilevile, tumefanya mabadiliko makubwa na kuboresha mitaala ya elimu ya awali, elimu ya msingi na elimu ya sekondari, pamoja na mafunzo ya ualimu,."--Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda
Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda, amesema katika mwaka wa fedha 2023/24 Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ilitekeleza vipaumbele vitano ambavyo ni:
(i) kukamilisha Mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 na Mitaala ya Elimu na kuanza utekelezaji wake kwa lengo la kuimarisha ujuzi kwa wahitimu;
(ii) kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa mafunzo ya amali (ufundi na mafunzo ya ufundi stadi) kwa sekondari na vyuo vya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi;
(iii) kuwezesha Ongezeko la fursa na kuimarisha ubora wa elimu ya msingi, sekondari na ualimu;
(iv) kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa elimu ya juu; na
(v) kuimarisha uwezo wa nchi katika tafiti, matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili kuchochea ujenzi wa uchumi wa viwanda.
"Katika kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia katika ngazi ya elimu ya msingi, sekondari na ualimu serikali itawezesha ujenzi wa shule za sekondari za kata 226, nyumba za walimu 184 wa sekondari na ununuzi wa vifaa vya maabara," -Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda
"Katika mwaka wa fedha 2024/2025 serikali itaongeza fursa za mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kutoka 223,201 hadi 252,245, pia serikali itatoa mikopo kwa wanafunzi 84,500 wa mwaka wa kwanza ambapo shahada ya kwanza 80,000, shahada za juu 2,000, wanaosoma nje ya nchi 500 na Samia Scholarship 2,000 na itatoa mikopo kwa wanafunzi 157,745 wanaoendelea na masomo," - Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda.
"Katika mwaka wa fedha 2024/25, Wizara imepanga kutekeleza vipaumbele vitano vyenye lengo la kuongeza ubora wa elimu kwa kuwezesha vijana wa Kitanzania kupata maarifa, ujuzi, kujiamini, kujiajiri na kuajirika, vipaumbele vyenye kujielekeza katika kutegemeza tafiti, sayansi, teknolojia na ubunifu katika ajenda ya maendeleo ya nchi," - Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda.
"Serikali imetoa mikopo kwa wanafunzi 2,299 wa ngazi ya stashahada yenye jumla ya shilingi bilioni 6,114,790,500.00," - Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda.
Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda ameliomba Bunge lipitishe bajeti ya wizara hiyo ya Sh. trilioni 1.965 kwa mwaka wa fedha 2024 /2025.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED