Wananchi watakiwa kuchukua tahadhari ya athari za mafuriko Kilombero

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 11:35 PM Apr 17 2024
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero,Dustan Kyobya akizungumza wakati akipokea msaada wa chakula kutoka Meneja wa Mawasiliano na Mahusiano wa Kampuni ya Sukari ya Kilombero,Victor Bemelwa.
Picha: Mpigapicha Wetu
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero,Dustan Kyobya akizungumza wakati akipokea msaada wa chakula kutoka Meneja wa Mawasiliano na Mahusiano wa Kampuni ya Sukari ya Kilombero,Victor Bemelwa.

Kutokana na Mvua zinazoendelea kunyesha katika wilaya ya Kilombero, Serikali imetoa wito kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhari za mvua hasa katika maeneo yanayotuamisha maji, ili kujikinga na athari za mvua zinazoendelea kujitokeza.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Dustan Kyobya wakati alipokuwa akipokea msaada wa chakula kutoka katika kiwanda cha sukari Kilombero kwa wananchi waliokumbwa na athari za Mvua zilizojitokeza katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo leo Aprili 17, 2024.

Naomba vyombo vya habari na kila mtu kwa nafasi yake kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kujenga uelewa wa pamoja katika kuchukua tahadhari za kukabiliana na athari za mvua zinazoendelea kujitokeza.Mvua zinaendelea kunyesha na athari za mvua ni kubwa kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri wasidharau maji yanayotiririka, alihimiza

“Tuchukue tahadhari kwa watoto wa shule wanahitaji uangalizi wa karibu lakini pia katika matumizi ya usafiri ambayo yanaweza kuleta madhara,” amesema Mkuu wa Wilaya Kyobya.

Aidha niwawashukuru kiwanda cha sukari kilombero kwa msaada mliotupatia na kwa kupitia Kamati ya Maafa ya Wilaya msaada huu utafikia walengwa waliokumbwa na athari za mvua.

“Nimefarijika namna mzigo ulivyogawanywa na kuhifadhiwa katika vifungashio hii imerahisisha zoezi la kusambaza kwa waathirika waliokumbwa na mafuriko ya mvua,” amesema Mkuu wa wilaya Kyobya.

Kwa upande wake Meneja wa Mawasiliano na Mahusiano wa Kampuni ya Sukari ya Kilombero, Victor Bemelwa amesema kampuni imeungana kuwashika mkono wananchi waliokumbwa na athari za mvua ikiwa ni wajibu wetu kurejesha katika jamii.

Tumekuja na msaada wa kibinadamu tukijua hitaji kubwa ni chakula kwa makundi ya watu waliokumbwa na kuathirika na mvua.

“Tumeleta tani 2 za unga wa mahindi tani 2 za maharage na tani 2 za mchele na tumezigawanya kwa kilo tano tano ili kusaidia kila kaya iliyoathirika mafuriko ya mvua na kwa mgawanyo tuliofanya tunaweza kusaidia kaya 500,” amesema Victor.

Tunatoa wito kwa asasi za kiraia na wadau wengine kuungana na sisi kushughulika na mambo au changamoto za jamii tunayohudumia.

Akizungumza katika upokeaji wa misaada, Mratibu wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu SACF- Ivo Alfred Ombela amesema watasimamia maelekezo ya Mkuu wa Wilaya kwa kushirikiana na Kamati ya Maafa ya Wilaya na kuhakikisha Misaada yote inayotoka kwa wadau na Serikalini inawafikia walengwa.

“Nitoe tahadhari kwa wale wanaoendelea na shughuli za ujenzi kuhakikisha wanaweka alama maeneo ambayo wameweka mashimo ili kusaidia timu za uokoaji kutopata madhara na kutumbukia katika maeneo hayo,” amesema Kamishina Ombela.

Ametoa wito kwa wananchi kutoa taarifa za mafaa yanapofika kwa kupiga no. 190 ambayo itapokelewa na kitengo cha Mawasiliano ya dharura cha Idara ya Menejimeti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Mji wa Ifakara, Zahara Muhidini Michuzi ameishukuru Kampuni ya Sukari ya Mvomero kwa msaada waliotoa kwa waathirika wa mvua za vuli zinazoendela kunyesha, amesema msaada umekuwa faraja na kututia moyo kuendelea na maisha yetu ya kila siku.

Mamlaka ya Hali ya hewa imetoa taarifa kwamba kuna Mvua Mpaka mwezi wa tano niombe wananchi kuendelea kuchukua tahadhari.