Msuya atoa somo kwa wajumbe wa Dira ya Maendeleo ya Taifa

By Imani Nathaniel , Nipashe Jumapili
Published at 04:13 PM May 26 2024
Aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais mstaafu, Cleopa Msuya.
Picha: Imani Nathaniel
Aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais mstaafu, Cleopa Msuya.

Aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais mstaafu, Cleopa Msuya, amesema kuwa umoja na ushirikiano kuwa ni nguzo mhimu katika kuleta mafanikio ya Dira ya maendeleo ya mwaka 2050 nchini.

Ameyasema hayo katika mjadala maalum uliongozwa na mjumbe wa  Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ya  Dk. Asha Rose Migiro, Dar es Salaam nyumbani kwake Upanga, ambapo ni mhimu kweka utaratibu wa kujifunza mbinu mbalimbali kwa nchi ambazo zimeendelea kiuchumi katıka kuhakikisha Tanzania inazidi kukua kiuchumi na kupata maendeleo.

Amesema katika kuelekea Dira hiyo, endapo vitu hivyo vitapewa kipaumbele vitasaidia katika sehemu kubwa ya kuliweka taifa kuwa  salama na amani bila ya kupata changamoto yoyote ile.

"Tuendelee kudumisha siasa za ndani  pamoja na za  kimataifa, huku jukumu linalotakiwa ikiwa ni  kuhakikisha nchi inakuwa salama, uchumi wa nchi unatokana na vile uwajibikiaji wako, umahiri na uhodari katika kazi siku zote,"alisema.

Alifafanua kuwa, jambo la muhimu ni kuthamini vilivyopo ndani na siyo kuiga kutoka mataifa mengine kwa kuwa, waasisi waliotangulia walikuwa wakihimiza kudumisha mila na desturi zilizokuwepo.

Kwa mujibu wa Dk. Msuya, alisema sekta ya kilimo, madini na viwanda zinasaidia sehemu katika sehemu kubwa ya ukuaji wa nchi kiuchumi.

Kwa upande wa Mjumbe wa Dira hiyo Balozi Dk. Asha Rose Migiro, alisema wamepokea maagizo hayo na kuhakikisha watayafanyia kazı, kwa lengo la kuendelea kusimamia utekelezaji wa Dira ya maendeleo ya mwaka 2050.

"Miongoni mwa mihimili tuliyoiweka katika majukumu yetu ni kuendelea kudumisha muungano na ushirikiano uliopo, tutaendelea kuangalia ni namna gani ya kujifunza kutoka nchi zilizopata maendeleo ili mafanikio yapatikane katika Dira yetu ya 2050,"alisema.

Naye Mkurugenzi wa ufuatiliaji na tathmini kutoka Tume hiyo, Dk. Mursali Milanzi , alimpongeza Msuya, kwa somo alilolitoa  kwa kuwa yatasaidia kuwapa mwongozo mzuri wanapokusanya taarifa mbalimbali zitakaosaidia kujua sehemu gani inayopaswa kupewa motisha.

Hata hiyo, Kamishna Msaidizi kutoka Wizara ya Madini, Mhandisi, Ally Samaje, alisema wataendelea kuwa na vipaumbele vya kutosha vitakavyosaidia wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao basi waendelee kufanya kazı kwa pamoja na ushirikiano siku zote.