Nishati Safi ya kupikia imebeba ajenda kubwa ya mazingira-Kapinga

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 10:51 AM May 18 2024
Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga.

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga, amewataka wananchi wa Msomera kuhakikisha wanaibeba ajenda ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo kuunga mkono jithada za serikali Ili kulinda mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Kapinga ameyasema hayo katika Kijiji cha Msomera Wilaya ya Handeni Mkoa wa Tanga kwenye hafla ya kugawa mitungi ya gesi na majiko banifu 1,500 iliyotolewa na REA na Taifa gesi, ikiwa ni mwendelezo wa juhudi za Wizara ya Nishati kugawa nishati safi ya kupikia kwa Watanzania na kuunga mkono jitihada za Rais, Dk. Samia  kufikisha asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.

"Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia ni ya Mhe.Rais mwenyewe na ndio kinara hivyo lazima tumuunge mkono kwa vitendo kwa kuacha kukata miti kwa ajili ya kupikia." alisema Kapinga.

Alisema ili kupata gunia moja la mkaa inahitajika magogo tani moja hadi mbili kupata nishati ya mkaa, hivyo amewataka wananchi wa Msomera kutumia kuni sasa basi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya  Handeni Wakili Albert Msando alisifu jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha watanzania wote wanatumia nishati safi ya kupikia na kuwataka wananchi wa Msomera kutumia  vema fursa ya majiko banifu na mitungi ya gesi.

Aidha Msando alimshukuru Naibu Waziri wa Nishati Kapinga kwa kuwafikishia mitungi ya gesi 1,500 na majiko banifu 1,500 ambapo awali waliomba 1,000, na kuomba  uwezekano  wa kuongezewa Ili kufikia kaya 3,400 za Msomera.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA Renatus Nkwabi alisema kuwa matakwa ya nishati safi ya kupikia ni ya watanzania wote na ndio maana REA imetoa majiko banifu kuunga mkono Serikali juu ya ajenda ya nishati safi ya kupikia  na kuwataka wananchi wa Msomera kuunga mkono jitihada hizo.

Jumla ya Kaya zaidi ya 3,000 za Wilaya ya Msomera zimepatiwa majiko banifu na mitungi ya gesi kuwezesha Kaya za wananchi wenye asili ya Kimasai waliohamia kutoka Ngorongoro kuja Msomera kunufaika na nishati safi ya kupikia, ikiwa ni mpango mkakati wa serikali wa miaka kumi uliozinduliwa hivi karibuni na Dkt.Samia Suluhu Hassan kuhakikisha matumizi ya nishati isiyo safi yanapunguzwa na kulinda mazingira na afya za watanzania.

Naye Meneja Mkuu wa Kampuni ya Taifa gesi ambao ndio waliotoa mitungi ya gesi kwa wananchi wa Msomera Davis Deogratius, aliahidi kuwasogezea huduma karibu wananchi wa Msomera ili kupata nishati safi ya kupikia kwa wakati

Aidha alimshukuru Naibu Waziri kwa kutimiza  ahadi yake ya kugawa nishati safi ya kupikia kwa wananchi wa Msomera na kuongeza kuwa wako Kama wadau wakubwa wa Nishati safi wataendelea kuunga mkono jitihada za serikali kuwapatia wananchi nishati safi ya kupikia 

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Wakurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Handeni na Msomera, Madiwani Kamati ya ulinzi na Usalama na wananchi wa wilaya ya Handeni na Msomera.