Rais Samia awapa tano wanawake wajasiliamali

By Vitus Audax , Nipashe Jumapili
Published at 03:37 PM May 19 2024
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akigawa tuzo za Malkia wa Nguvu 2024 kwa Wanawake 10 Wapambanaji wa Kanda ya Ziwa.
Picha: Mwandishi Wetu
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akigawa tuzo za Malkia wa Nguvu 2024 kwa Wanawake 10 Wapambanaji wa Kanda ya Ziwa.

RAIS Samia Suluhu Hassan amewapongeza wanawake wote nchini wanaojihusisha na shughuli za biashara na ujasiriamali katika sekta mbalimbali na kuwataka kuendelea na uwajibikaji wao ipasavyo ili kuinua uchumi wao na kuongeza pato la Taifa kwa ujumla.

Pongezi hizo za Rais Samia zilitolewa mkoani Mwanza na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, katika usiku wa Malikia wa Nguvu Kanda ya Ziwa unaosimamiwa na Clouds Media Group (CMG).

"Kama nilivyowaambkia kuwa tukio hili linafuatiliwa mbashara na nchi nzima, lakini pia Malkia wa Nguvu nambari moja Dk.Samia Suluhu Hassan yupo kwenye TV anaangalia tukio hili na nikiwa hapa amenipigia simu na kuniambia nakuona hapo Mwanza,”

“Kwahiyo amenituma niwasalimu Malkia wote na ameniambia nifikishe salamu hizi za pongezi kwenu kwani ameona namna ambavyo mnajishughulisha kwenye mkakati wa kiuchumi na amafurahi kuona sasa akina mama mnajiamini na kusimamia shughuli zenu,” amesema Majaliwa.

Amesema Rais Samia ameahidi kuendelea kuwa pamoja nao katika kuhakikisha wanawajibika ipasavyo ili kujiinua kiuchumi na kuinua pia pato la Taifa.

Aidha Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa wananwake nchini kutumia Mitandao ya kijamii kutangaza biashara na ubunifu wao ili kujiimarisha na kukuza mitaji yao kwa kuongeza wigo wa wateja wanaopatikana kwa haraka.

Amewataka wanawake kutumia kikamilifu fursa zilizopo nchini kwani tayari Serikali imeweka mifumo ya kurahisisha uwekezaji pamoja na kuboresha mifumo ya kuwainua wanawake katika kukuza shughuli zao za uchumi za kila siku.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tuzo hizo,Liliane Masuka amesema kwa mwaka huu wanatarajia kuziendesha kwa kipindi cha miezi nane na kuwafikia wanawake zaidi ya milioni nane.

Amesema lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha wanaunda ajira mpya,kuinua uwezo mpya wa kibiashara miongoni mwa wanawake pamoja na kutoa mchango katika kukuza pato la Taifa.

Kati ya waliopata tuzo katika usiku huo ni pamoja na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) Nelly Msuya aliyepata tuzo kinara sekta ya utumishi wa umma.