NBC yasisitiza dhamira yake kuendeleza kuunga mkono jitihada za Serikali za Mitaa

By Hawa Abdallah , Nipashe
Published at 09:49 PM Apr 23 2024

Waziri wa TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa  (wa pili kushoto) akikabidhi cheti cha utambuzi na shukrani kwa Mkurugenzi wa wateja wakubwa na Shughuli za Serikali wa NBC ,James Meitaron (wa pili kulia) ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa benki hiyo.
Picha: Mpigapicha Wetu
Waziri wa TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa (wa pili kushoto) akikabidhi cheti cha utambuzi na shukrani kwa Mkurugenzi wa wateja wakubwa na Shughuli za Serikali wa NBC ,James Meitaron (wa pili kulia) ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa benki hiyo.

Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imesisitiza dhamira yake ya kuunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa na Mamlaka za Serikali za Mitaa (LGAs) katika kuwawezesha na kukuza maendeleo endelevu kwa manufaa ya jamii.

Adhma hiyo ya benki ya NBC imetangazwa na Mkurugenzi wa wateja wakubwa na Shughuli za Serikali wa NBC , James Meitaron wakati akizungumza kwenye Mkutano Mkuu wa 38 wa Mwaka wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) unaofanyika Zanzibar. Benki ya NBC ni moja ya wadhamini muhimu wa mkutano huo uliozinduliwa leo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa.

Akizungumza kwenye mkutano huo Meitoron amewasilisha pongezi za benki hiyo iliyoonesha kukubaliana na jitihada mbalimbali zinazofanywa na mamlaka za mitaa katika kuendesha maendeleo ya kiuchumi nchini Tanzania. Amesisitiza ahadi ya NBC  katika kutoa suluhisho za kibenki zilizokusudiwa kukidhi mahitaji ya mamlaka hizo.
“Mchango mkubwa wa NBC katika uchumi wa taifa dhahiri ambapo takriban Sh. 66.5 bilioni zilipelekwa katika hazina ya taifa pekee mwaka 2023. Ni fahari kwetu kuwa sehemu muhimu ya safari ya maendeleo ya Tanzania na tutaebdelea kusaidia mamlaka za serikali za mitaa na jamii kwa ujumla,’’ amebainisha Meitoron

Kwa mujibu wa Meitaron, benki hiyo imekuwa ikitoa huduma mbalimbali za kibenki kwa njia ya kielektroniki zilizoundwa kwa ajili ya kuboresha ukusanyaji mapato na mchakato wa malipo kwa Serikali na Halmashauri za Miji. Huduma hizo ni pamoja na huduma ya malipo mbalimbali kwa serikali kupitia mfumo wa yaani GePG, NBC Wakala, mashine za POS, na huduma ya Benki kupitia Simu na Intaneti ambazo zinasaidia kuongeza ufanisi na uwazi katika masuala ya kifedha.

“Zaidi ya hayo ushiriki wa NBC katika ufadhili na ujenzi wa miradi mikubwa muhimu kama reli ya SGR na Hati fungani ya Kijani ya Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira ya Jiji la Tanga, ikionyesha nafasi yake katika kusaidia maendeleo ya miundombinu ya taifa. Zaidi tunaunga mkono vikundi maalum vikiwemo vya wajasiriamali (SMEs), mnyororo wa thamani ya kilimo, na kampuni changa,’’ ametaja.

Amesisitiza dhamira ya benki hiyo katika kutoa mikopo mikubwa, Meitaron ametolea mifano mkopo ya dola milioni 200 kwa Serikali ya Zanzibar na mpango wa fedha ya dhamana ya miji. Alikaribisha taasisi za serikali zinazohitaji uwezeshaji wa kifedha kwa miradi muhimu, akisisitiza utaalamu na uwezo wa NBC katika kurahisisha jitihada hizo.
Meitaron amezihakikishia mamlaka hizo kuwa benki hiyo iko tayari kuzihudumia mahitaji yao ya kifedha.
“Kama benki inayomilikiwa na serikali na mshirika wa kuaminika katika maendeleo ya kitaifa, NBC iko tayari kuziwezesha mamlaka za serikali za mitaa kwa kuzipatia huduma maalum kwa ajili ya kuongeza mapato na ukuaji endelevu.’’ amesema.