Makonda awataka watendaji kuongeza kasi kuwahudumia wananchi

By Beatrice Shayo , Nipashe
Published at 04:37 PM May 09 2024
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda.
Picha: Beatrice Shayo
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda, amewataka watendaji na watumishi wa ofisi yake wanaosikiliza wananchi pamoja na mawakili wanaotoa msaada wa kisheria kwa wananchi kuongeza kasi katika kuhudumia wananchi.

Makonda aliyasema hayo leo wakati akizungumza na wananchi waliojitokeza kutatuliwa kero zao ambapo aliwataka watendaji hao kuhakikisha wananchi wote wanasikilizwa na kutatuliwa kero zao.

Aidha, Makonda amewaambia wananchi kuwa nafasi, cheo chake na nguvu zake zote amezielekeza kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha ambao wamesahulika katika kupata haki na watumishi wasiokuwa waaminifu na wananchi wenye fedha.

Amesema amefarijika kwa wingi wa wananchi waliojitokeza ofisini kwake licha ya mvua kubwa kunyesha tangu majira ya asubuhi.

Aidha,  Makonda ameonesha kushangazwa na baadhi ya watu wanaokosoa kliniki yake ya kuwasikiliza wananchi na kuwaambia kuwa nafasi yake siku zote ataitumia kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wananufaika.